1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Viongozi wa Afrika kukutana tena na Rais Jammeh

Sylvia Mwehozi
10 Januari 2017

Ujumbe wa viongozi wa nchi za Afrika Magharibi unatarajiwa kukutana kwa ajili ya kujaribu kumshawishi rais wa Gambia Yahya Jammeh kuachia madaraka lakini ukasema matumizi ya nguvu za kijeshi bado ni hatua inayofikiriwa.

Nigeria Ecowas-Treffen
Picha: Getty Images/AFP/P.-U. Ekpei

Rais wa Nigeria Muhammadu Buhari ataongoza ujumbe huo katika mji mkuu wa Gambia wa Banjul hapo kesho Jumatano kujadiliana na rais Jammeh, akiongozana na marais wenzake wa Afrika Magharibi, rais wa kamisheni ya ECOWAS, mwakilishi maalum wa Umoja wa Mataifa na pia mwakilishi wa Umoja wa Afrika.

Matumizi ya nguvu za kijeshi

Waziri wa mambo ya nje wa Nigeria, Geoffrey Onyeama, amesema ujumbe huo utamtaka rais Jammeh "kuheshimu katiba", wakati muhula wa miaka mitano wa kiongozi huyo utakapomalizika Januari 18 lakini mpaka sasa amekataa kuyakubali matokeo ya uchaguzi wa mwezi Desemba ambapo rais mteule Adama Barrow alishinda. "Wamekubaliana juu ya dhamira ya kutatua mgogoro wa kisiasa wa Gambia kwa namna ambayo katika kila hatua ya mchakato itakayofuata katiba ya Gambia na inaheshimu matakwa ya watu wa Gambia."

Rais wa sasa wa Gambia Yahya Jammeh Picha: Getty Images/AFP/I. Sanogo

Jumuiya ya kiuchumi ya nchi za Afrika Magharibi ECOWAS inaweza kuingilia kati kijeshi ikiwa kiongozi huyo atashindwa kuachilia madaraka na kwamba wamejiandaa kutumia chaguo lolote ambalo wanahisi ni sahihi kutekeleza mchakato wa katiba, amesema  waziri wa mambo ya nje wa Nigeria Geoffrey Onyeama.

Kufutwa kazi

Wakati hayo yakitarajiwa rais Yahya Jammeh amemfuta kazi waziri wake wa mawasiliano, Sheriff Bojang, na nafasi yake kuchukuliwa mbunge aliyechaguliwa mwezi huu kama msemaji wa chama tawala.

Chanzo kutoka wizara ya mambo ya nje, kimesema kwamba kiongozi huyo pia amewafukuza kazi mabalozi katika mataifa 12 kwa kile kilichotajwa ni kukosa utiifu. Mabalozi hao walimuunga mkono Barrow mwishoni mwa Desemba na kumtaka rais huyo kuachia madaraka.

Rais mteule wa Gambia Adama Barrow Picha: picture-alliance/AA/X. Olleros

Mamlaka zimekataa pia kumuachia kutoka mahabusu mkurugenzi wa zamani wa Televisheni na radio ya taifa licha ya uamuzi wa mahakama wa kumpatia dhamana. Wakati huo huo imeoneka dhahiri kuwa hakutakuwa na idadi kamili ya majaji wanaohitajika Jumanne hii katika mahakama kuu kusikiliza kesi ya Jammeh dhidi ya Tume huru ya uchaguzi IEC.

Majaji watano kutoka Nigeria na mmoja wa Sierra Leonne walialikwa kusikiliza kesi hilo lakini mpaka sasa hakuna aliyejitokeza. Gambia inategemea majaji wa kigeni kutokana na uhaba wa watalaamu hao wenye mafunzo na uzoefu unaohitajika.

Jammeh na chama chake wamewasilisha mashitaka matatu ya kisheria tofauti katika mahakama hiyo wakilalamika udanganyifu wa kuhesabu kura na tume ya uchaguzi pamoja na vitisho dhidi ya wafuasi wake.

Mwandishi: Sylvia Mwehozi/AFP

Mhariri: Yusra Buwayhid

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW