1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

G7 kutoa dola bilioni 5 kukabili kitisho cha njaa

28 Juni 2022

Mkutano wa kilele wa viongozi wakuu wa mataifa saba yaliostawi zaidi kiuchumi duniani, G7 umekamilika kwa ahadi ya kukabiliana na njaa duniani na mabadiliko ya tabia nchi pamoja na kuisadia Ukraine dhidi ya Urusi.

Deutschland | G7 Gipfel | PK Olaf Scholz
Picha: Leonhard Foeger/REUTERS

Viongozi wakuu wa nchi na serikali wa kundi la nchi tajiri kiviwanda duniani G7 wanatarajiwa kutoa ahadi  ya dola bilioni tano kuimarisha usalama wa chakula duniani,miongoni mwa hatua nyingine,wakati wakikamilisha mkutano wao wa kilele unaofanyika huko Kusini mwa Ujerumani.

Hatua ya viongozi wa kundi la G7 ni jibu la wasiwasi unaojitokeza katika nchi zinazoendelea  kuhusu kitisho cha kuzuka njaa kilichochochewa na vita vya Ukraine.Kadhalika viongozi hao wanashughulika kutafuta njia za kuisadia Ukraine kusafirisha nafaka zake kwa mujibu wa waziri mkuu wa Uingereza Boris Johnson.

Soma pia: Viongozi wa G7 waapa kuisaida Ukraine "bila kuchoka"

Tangazo hilo la waziri mkuu Johnson amelitowa leo mwanzoni mwa mkutano wa pembezoni wa pande tano na viongozi wa Ufaransa, Emmanuel Macron, Mario Draghi wa Italia, kansela wa Ujerumani Olaf Scholz na rais wa Marekani Joe Biden.

Mpaka sasa Ukraine imeshindwa kusafirisha nafaka zake ikizuiwa na vizuizi vilivyowekwa na Urusi katika bandari zake za bahari nyesi,hatua ambayo imewalazimisha wasafirishaji kutumia njia za nchi kavu ambazo hazina uhakika.

Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz akihutubia waandishi habari kuhusu maazimio la mkutano wa kilele wa wakuu wa mataifa ya kundi la G7, mjini Elmau, Ujerumani.Picha: Leonhard Foeger/REUTERS

Lakini pia   Kundi hilo la viongozi wa nchi saba tajiri kiviwanda linakamilisha mkutano wake huo wa kilele leo Jumanne,mkutano ambao ulikuwa na nia ya kutuma ujumbe mzito wa kuonesha kujitolea kwa nchi hiyo katika kuiunga mkono Ukraine na mustakabali wake.

Lakini pia kuihakikishia Urusi kwamba italipia gharama kubwa  kutokana na hatua yake ya kuivamia Ukraine na bila shaka pia kuutafutia ufumbuzi mgogoro wa njaa duniani na kuonesha mshikamano katika mapambano dhidi ya mabadiliko ya tabia nchi.

Soma pia: Kongamano la G7 Elmau, Ujerumani: Je ni zaidi ya onyesho?

Kabla ya kumalizika mkutano huo viongozi hao wameungana kulaani shambulizi la Urusi dhidi ya jengo la maduka katika mji wa Kremechuk na kukiita kitendo hicho cha Urusi kuwa uhalifu wa kivita na kuahidi kwamba rais Vladmir Putin na wengine wanaohusika watabebeshwa dhamana.

Marekani imeelezwa kwamba itachangia zaidi ya nusu  ya dola bilioni 5 zilizoafikiwa na kimsingi fungu hilo litatumika kusaidia juhudi za kuimarisha usalama wa chakula katika nchi 47, kuokoa maisha kupitia shughuli za moja kwa moja za msaada wa kibinadamu,pamoja na kuimarisha mifumo ya uzalishaji chakula kote duniani na hasa katika maeneo yaliyoko hatarini.

Viongozi wakuu wa G7 kutoka kushoto, waziri mkuu wa Uingereza Boris Johnson, rais wa Marekani Joe Biden, kansela wa Ujerumani Olaf Scholz, rais wa Ufaransa Emmanuel Macron, na waziri mkuu wa Italia Mario Draghi, wakikutana kandoni mwa mkutano mkuu wa kilele wa G7 katika kasri la Elmau, mjini Kruen, Jumanne 28, 2022.Picha: Susan Walsh/AP/picture alliance

Vita vya Ukraine ambavyo hivi sasa vimeingia mwezi wake wa tano vinasababisha hali ngumu ya kusafirishwa nafaka kutoka bandari za nchi hiyo na kuchochea ongezeko kubwa la bei ya vyakula dunia nzima. Na wataalamu na mashirika ya msaada wanatahadharisha juu ya kutokea uwezekano wa baa la njaa katika baadhi ya maeneo ya Afrika.

Soma pia: Biden: Lazima tusimame pamoja dhidi ya Urusi

Viongozi wa kundi la G7,linazijumuisha Uingereza,Canada,Ufaransa,Ujerumani,Italia, Japan na Marekani wametangaza azimio la pamoja linalojumuisha  hatua iliyopigwa katika mkutano wao wa kilele katika hoteli ya kifakhari ya Schloss Elmau ambapo kansela Olaf Scholz anatarajiwa kuwa na mkutano na waandishi habari.

Viongozi hao wameonesha mshikamano mbele ya uvamizi wa Urusi nchini Ukraine na kuonekana kupiga hatua kiasi fulani kuhusu masuala kadhaa ikiwemo  kupunguza utegemezi wa nishati kutoka Urusi na  hatua za kuiadhibu nchi nchi hiyo pamoja na kuunga mkono juhudi za Ukraine katika vita hivyo.

Mkutano wa G7 waanza Canada

00:52

This browser does not support the video element.

Soma pia: G7 yaweka hazina ya miundombinu kwa nchi zinazostawi

Juu ya hayo afisa kutoka Ikulu ya Marekani amesema kuna uwezekano viongozi wa G7 wakawapa majukumu mawaziri wao kuanzisha mchakato wa utaratibu wa kuweka viwango maalum katika bei ya mafuta kutoka Urusi. Ingawa kwenye mkutano huo wa kilele wakosoaji walitowa hoja kwamba hatua hiyo itakuwa vigumu kuitekeleza. Viongozi wa G7 wanajaribu kuizuia Urusi kutopata faida kutokana na ongezeko la bei.

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW