Vita vya Iran vyatishia kuacha urithi wa sumu kwa mazingira
12 Machi 2026
Mashambulizi dhidi ya miundombinu ya mafuta na vituo vya makombora katika vita kati ya Marekani na Israel dhidi ya Iran yameibua wasiwasi miongoni mwa wataalamu kuhusu urithi wa sumu kwa afya ya binadamu na mazingira ambao unaweza kudumu muda mrefu hata baada ya mzozo kumalizika.
Tangu mzozo huo uanze, shirika lisilo la kiserikali lenye makao yake Uingereza la Conflict and Environment Observatory (CEOBS) limetambua zaidi ya matukio 300 yanayoweza kusababisha uharibifu wa mazingira — kuanzia mashambulizi ya vituo vya makombora hadi mashambulizi dhidi ya meli za kubeba mafuta katika Ghuba ya Uajemi.
Hata hivyo, watafiti wanasema idadi hiyo huenda ni sehemu ndogo tu ya uharibifu uliotokea.
"Hicho ni kilele tu cha barafu,” alisema mkurugenzi wa CEOBS, Doug Weir, akizungumza na DW. "Marekani inadai imepiga maeneo 5,000. Kwa sasa, bado tunagusa juu juu tu.”
Umoja wa Mataifa pia umeonya kuwa mashambulizi ya hivi karibuni dhidi ya miundombinu ya mafuta yanaweza kusababisha "madhara makubwa ya kimazingira katika eneo lote, ikiwa ni pamoja na athari za haraka kwa maji salama, hewa inayohitajika kuvutwa na watu, na chakula.”
Dalili moja ya hatari hizo ilionekana wakati "mvua nyeusi” — mchanganyiko wa mafuta na mvua — ilipofunika barabara za Tehran kufuatia mashambulizi ya Israel mwishoni mwa wiki dhidi ya vituo kadhaa vya mafuta.
Moto katika vituo hivyo ulipeleka moshi mzito mweusi juu ya mji mkuu huo wenye wakazi karibu milioni 10, na kusababisha Shirika la Msalaba Mwekundu la Iran kuwaonya wakazi wabaki majumbani ili kuepuka hewa yenye sumu. Baadhi ya wakazi waliripoti maumivu ya kichwa na matatizo ya kupumua.
Moshi huo huenda ulikuwa na vichafuzi "ikiwemo chembechembe ndogo hewani na dioksidi ya salfa, pamoja na misombo tete yenye sumu na bidhaa hatari za mwako,” alisema Zongbo Shi, profesa wa baiogeokemia ya anga katika Chuo Kikuu cha Birmingham, Uingereza.
Chembe hizo zinaweza kupenya ndani kabisa ya mapafu na kuhusishwa na ongezeko la hatari ya magonjwa ya mfumo wa kupumua na moyo, hasa kwa watoto wachanga, wazee na watu wenye matatizo ya kiafya yaliyokuwepo tayari, aliongeza Shi.
Mabomu: Urithi mrefu wa sumu
Mbali na uchafuzi wa hewa wa mara moja, wataalamu wanaonya kuwa maeneo ya kijeshi na nishati yaliyoshambuliwa yanaweza kuacha uchafuzi unaodumu kwa miaka mingi.
Vituo vya mafuta vinaposhambuliwa— kama ilivyotokea Iran na katika mataifa mengine ya Ghuba — vinaweza kuachilia mawingu ya vichafuzi vyenye sumu vinavyoweza kusambaa hadi jamii za karibu na kujikusanya barabarani, juu ya paa, kwenye udongo na mashamba ya mazao, kwa mujibu wa CEOBS.
Mashambulizi dhidi ya maeneo ya kijeshi kama vituo vya makombora yanaweza pia kuwa hatari sana, kwani moto na milipuko hueneza sumu kama mafuta ya ndege, metali nzito, kemikali za PFAS na vilipuzi. Baadhi ya vitu hivyo vinaweza kubaki katika mazingira muda mrefu baada ya vita kumalizika.
Kwa mfano, TNT inayotumika katika silaha na inayochukuliwa kuwa inaweza kusababisha saratani kwa binadamu kulingana na Wakala wa Ulinzi wa Mazingira wa Marekani (EPA), inaweza kubaki kwenye udongo na kuathiri mimea na afya ya watu.
Hata hivyo, ni vigumu kutathmini kiwango cha uchafuzi bila vipimo vya moja kwa moja katika maeneo husika.
"Kuna ukosefu mkubwa wa uwazi na uhakika kuhusu kilichopo katika maeneo yaliyoshambuliwa,” alisema Weir. "Tunajua kwa ujumla yanaweza kuwa na vifaa vya kijeshi vyenye sumu kama mafuta ya makombora, lakini hatuna maelezo au data sahihi kuhusu kilichoharibiwa.”
Kundi lake hutumia tu picha za satelaiti, ramani za uharibifu wa rada, mitandao ya kijamii na ripoti za habari kutathmini hatari za mazingira kwa mbali.
Mifumo ya bahari hatarini
Mashambulizi ya Marekani na Israel dhidi ya jeshi la majini la Iran pamoja na mashambulizi ya Tehran dhidi ya meli zinazopitia Mlango wa Hormuz pia yanaongeza hatari ya kumwagika kwa mafuta baharini.
Ghuba ya Uajemi ina miamba mingi ya matumbawe na mifumo muhimu ya bahari, ikiwemo nyasi za baharini zinazotoa makazi kwa samaki, chaza wa lulu, kasa wa kijani na idadi ya pili kwa ukubwa duniani ya dugong walio hatarini kutoweka. Jamii nyingi za wavuvi pia hutegemea dagaa kutoka katika maji hayo.
"Hiki ni kipengele ambacho hatukioni sana katika migogoro mingi,” alisema Weir. "Pia tumeshuhudia maeneo kadhaa ya pwani yakishambuliwa na Israel, ambapo kuna uwezekano mkubwa wa vichafuzi kuingia katika mazingira ya pwani.”
Marekani ilisema Jumatano kuwa imezamisha zaidi ya meli 60 za Iran wakati wa mashambulizi.
Meli zinazozama zinaweza kuwa chanzo cha muda mrefu cha uchafuzi ikiwa mafuta au kemikali nyingine hatari zitavuja kwenye maji yanayozunguka, alisema Weir. Aliongeza kuwa frigeti ya Iran iliyopigwa wakati wa mzozo sasa inavuja mafuta yanayoacha doa refu la kilomita kadhaa karibu na Sri Lanka.
"Sio Ghuba ya Uajemi pekee iliyo hatarini,” alibainisha Weir. "Athari hizi za kimazingira sasa zimefika hadi Sri Lanka.”
Vita vina alama kubwa ya hewa ukaa
Njia nyingine ambayo athari za kimazingira zinaweza kuenea nje ya maeneo ya mapigano ni kupitia uzalishaji mkubwa wa gesi chafuzi unaosababishwa na vita.
Kwa mfano, miaka mitatu ya kwanza ya vita vya Urusi nchini Ukraine ilisababisha takribani tani milioni 230 za CO2, kulingana na shirika lisilo la kiserikali la Initiative on GHG Accounting of War — sawa na uzalishaji wa pamoja wa kila mwaka wa Hungary, Austria, Czechia na Slovakia.
Jeshi lenyewe hutumia sana nishati ya visukuku. Kama majeshi yote duniani yangekuwa nchi moja, yangekuwa ya nne kwa uzalishaji mkubwa wa hewa ukaa duniani, yakichangia takribani asilimia 5.5 ya uzalishaji wa kimataifa.
Hata hivyo, mataifa hayalazimiki kujumuisha uzalishaji wa kijeshi katika takwimu za kitaifa wanazowasilisha chini ya makubaliano ya Paris kuhusu mabadiliko ya tabianchi.
Linapokuja suala la urithi wa kimazingira wa vita, mara nyingi umakini huwa kwa mambo yanayoonekana wazi, alisema Weir.
"Tunaona moto, milipuko, mashimo ardhini, harakati za magari ya kijeshi, na mamilioni ya kilomita za nyaya za mawasiliano zikitandazwa misituni au kwenye mstari wa mbele — kama tunavyoona Ukraine kwa sasa,” alisema.
Changamoto za kurejesha mazingira baada ya vita
Iran tayari ilikuwa inakabiliwa na shinikizo kubwa la kimazingira, ikiwemo uhaba sugu wa maji, uchafuzi unaoongezeka wa hewa na kuharibika kwa mifumo mikuu ya ikolojia, hali iliyochochewa na mabadiliko ya tabianchi na usimamizi dhaifu wa serikali.
Vita vinaongeza changamoto hizo. Migogoro mara nyingi hufuatwa na udhaifu wa utawala, ambapo ulinzi wa mazingira hupewa kipaumbele cha chini wakati wa mpito kutoka vita hadi amani, alibainisha Weir.
Anaamini hali hiyo inaweza kutokea pia Iran — nchi ambayo alisema kwa kawaida "imekuwa na usiri mkubwa kuhusu masuala ya mazingira na uharibifu wake.”
Iwapo utawala wa Iran utaendelea kuwepo, haijulikani wazi utakuwa wazi kwa kiasi gani kuhusu hitaji la kusafisha mazingira au kiwango cha msaada kitakachopatikana kutoka kwa jumuiya ya kimataifa.
"Tunaona uharibifu mkubwa wa mazingira, lakini pia kuna uwezekano mkubwa kwamba kutakuwa na ukosefu wa uwazi kuhusu hilo siku zijazo na uwezo mdogo wa kusafisha au kudhibiti madhara yaliyosababishwa,” alisema.