1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Von der Leyen atoa wito wa Umoja kati ya Ulaya na AU

Sekione Kitojo
7 Desemba 2019

Rais wa Halmashauri ya Umoja wa Ulaya Ursula von der Leyen Jumamosi alitoa wito wa kuwepo na usalama zaidi na  kupungua kwa uhamiaji kinyume na utaratibu wakati wa ziara yake mjini Addis Ababa, Ethiopia.

Äthiopien Ursula von der Leyen  Addis Ababa
Picha: Reuters/T. Negeri

 

Mji  huo  ni makao  makuu  ya  Umoja  wa  Afrika (AU).

"Ni umoja  tu  ndio utaweza  kufanya  mabara  yetu  kuwa  yenye nguvu  katika  kubadilisha  dunia. Umoja  wa  Afrika  ni  mshirika namba  moja  ambae naweza kumtegemea,"  von der Leyen amesema  wakati  wa  ziara  yake  nje  ya  bara  la  Ulaya  kama kiongozi  mkuu wa  halmashauri tendaji  ya  Umoja  wa  Ulaya.

Makao makuu ya Umoja wa Afrika mjini Addis AbabaPicha: DW/B. Riegert

Amesema  hatawasilisha "mpango  mkubwa  kwa  Afrika," lakini  yuko nchini  Ethiopia "kusikiliza" jinsi hali  inavyokwenda  na maendeleo yanayolijenga  bara  hilo,  pamoja  na  malengo  yake katika  siasa na  uchumi.

Von der Leyen alianza  ziara   yake  kwa  mkutano  pamoja  na mwenyekiti  wa  halmashauri  ya  Umoja  wa  Afrika Moussa Faki pamoja  na  makamishina  wengine. Pia  amepangiwa  kukutana  na waziri  mkuu  wa  Ethiopia  Abiy Ahmed, ambaye  hivi  karibuni alipata  tuzo  ya  amani  ya  Nobel, na  rais  wa  Ethiopia  Sahle-Work Zewde.

Von  der Leyen ameelezea  kuhusu  ushirikiano wa  kimkakati  na Afrika  kuwa  moja  katika  malengo  yake makuu  ya  masuala  ya kigeni, akilielezea bara  hilo  kuwa  ni "jirani yao wa  karibu na mshirika  wake wa  asili."

Halmashauri  anayoiongoza  von der Leyen  itahitaji  kufanyakazi na matifa  ya  Afrika kutimiza lengo  muhimu  la  sera ya kushughulikia uhamiaji, suala  linaloleta  utata miongoni  mwa  mataifa  wanachama wa  Umoja  wa  Ulaya.

Rais wa halmashauri ya Umoja wa Ulaya Ursula von der Leyen akikaribishwa katika makao makuu ya AU na mwenyekiti wa halmashauri ya Umoja huo Moussa FakiPicha: Reuters/T. Negeri

Sehemu  kubwa  ya  wahamiaji  ambao wanawasili   katika  mataifa ya  Umoja  wa  Ulaya  bila  utaratibu  maalum  wanatoka  mataifa  ya Afrika  kusini  mwa  jangwa  la  Sahara, kwa  mujibu  wa  data za umoja  huo.

Moja kati  ya  mikakati  mipya  ya  halmashauri  hiyo  kuzuwia uhamiaji ni  kuimarisha hali  za  watu  katika  mataifa  wanayotoka kwa  kufanya  uwekezaji  wa kikanda. Mkakati  mwingine  ni kuimarisha mpaka  wa  Umoja  wa  Ulaya  na  shirika la  ulinzi  wa pwani  la Frontex.