1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waandamanaji wadai ushindi Uturuki

2 Juni 2013

Maelfu ya waandamanaji wameshangiria ushindi mapema leo Jumapili(02.06.2013) baada ya polisi kuondoka kutoka katika eneo la uwanja uliohusika na maandamano makubwa dhidi ya serikali nchini Uturuki.

Demonstrators shout slogans during an anti-government protest in Istanbul June 1, 2013. Turkish Prime Minister Tayyip Erdogan called for an immediate end on Saturday to the fiercest anti-government demonstrations for years, as protesters clashed with riot police in Istanbul for a second day. REUTERS/Murad Sezer (TURKEY - Tags: POLITICS CIVIL UNREST)
Waandamanaji wakiimba kauli mbiu mjini IstanbulPicha: Reuters

Makundi ya haki za binadamu yameshutumu matumizi ya nguvu yaliyofanywa na polisi, huku shirika la Amnesty International likisema kuwa watu wawili wameuawa, wakati mataifa washirika wa Uturuki ya magharibi Uingereza na Marekani zikitoa wito kwa serikali kuonesha uvumilivu.

Uwanja wa Taksim umekuwa katikati ya wimbi la maandamano ambayo yamesababisha watu kadha kujeruhiwa, kwa mujibu wa Amnesty International mamia wamejeruhiwa, ambapo pia baadhi ya waandamanaji wamebakia kuwa hawaoni kutokana na gesi ya kutoa machozi kutokana na mabomu ya polisi.

Waandamanaji wamefyatuliwa bomu la kutoa machozi mjini AnkaraPicha: Reuters

Waandamanaji watamba

Jioni ya Jumamosi, hata hivyo, waandamanaji walicheza na kuimba katika uwanja huo baada ya polisi kujiondoa kutoka katika eneo hilo, na wengine kufyatua fataki katika kusherehekea.

"Serikali ijiuzulu!" waandamanaji walipiga kelele wakati polisi wakirejea nyuma. "Tuko hapa tayyip, wewe uko wapi?" Waliimba , wakimbeza waziri mkuu Recep Tayyip Erdogan.

Waziri mkuu wa Uturuki Recep Tayyip ErdoganPicha: picture-alliance/dpa

Kile kilichoanza kama malalamiko dhidi ya mradi wa serikali ya mtaa umeingia katika maandamano makubwa dhidi ya kile wakosoaji wanachosema kuwa ni agenda ya uhafidhina na mkono wa chuma.

Ghasia zasambaa

Tangu mapambano ya mwanzo siku ya Ijumaa, ghasia zimesambaa katika miji mingine nchini humo. Jana Jumamosi(01.06.2013), polisi mjini Ankara walilizuwia kundi la waandamanaji kulifikia jengo la bunge pamoja na ofisi ya waziri mkuu.

Waandamanaji mjini IstanbulPicha: Reuters

Erdogan amekiri katika hotuba kuwa kumekuwa na hatua nyingine za matumizi ya nguvu kupita kiasi kwa polisi.

Lakini ameongeza: "Nawatolea wito waandamanaji kuacha maandamano mara moja." Wizara ya mambo ya ndani imesema kuwa hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi ya maafisa wa polisi ambao wamefanya mambo ambayo ni kinyume na sheria.

Erdogan alikuwa akizungumza wakati machafuko hayo yakiendelea kwa siku ya pili mfululizo katika uwanja wa Taksim, eneo maarufu la kitalii na kwa kawaida hutumika pia kwa mikutano mjini Istanbul.

Polisi wakiwamwagia waandamanaji maji ya kuwashaPicha: Reuters

Hata hivyo waandamanaji wamewasha mioto na kupambana na polisi katika baadhi ya sehemu za mji wa Istanbul na Ankara mapema leo Jumapili, lakini mitaa imekuwa kwa wastani shwari baad ya siku mbili za maandamano makubwa na ghasia nchini Uturuki dhidi ya serikali ya nchi hiyo.

Mwandishi: Sekione Kitojo / rtre / afpe

Mhariri : Bruce Amani.

Ruka sehemu inayofuata Gundua zaidi
Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW