1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wabunge wa Denmark wapitisha sheria ya kuomba hifadhi

Tatu Karema
3 Juni 2021

Wabunge nchini Denmark Alhamisi wamepiga kura kuidhinisha kuanzishwa kwa kituo cha kupokea wakimbizi katika nchi ya tatu ambayo huenda ikawa barani Afrika.

Dänemark Ministerpräsidentin Mette Frederiksen
Picha: Imago Images/Ritzau Scanpix/L. Sabroe

 

Wabunge waliidhinisha sheria hiyo kwa kura 70 dhidi ya 24 za hapana, na wabunge 85 ambao hawakuwepo wakitoa idhini kwa serikali kuwahamisha watafuta hifadhi katika taifa la tatu pindi makubaliano yatakapofikiwa kwa lengo la kushughulikia kwa haraka maombi ya hifadhi na ulinzi wowote utakaofuatia kwendana na majukumu ya kimataifa ya Denmark.

 

Kamishna wa Umoja wa Mataifa anaeshughulikia wakimbizi, Umoja wa Ulaya na mashirika kadhaa ya kimataifa wamekosoa mpango huo, wakisema utadhoofisha ushirikiano wa kimataifa na unakosa ufafanuzi kuhusu namna haki za binadamu zitakapolindwa. Lakini waziri wa Uhamiaji Mattias Tesfaye, amesema serikali ya Denmark ilihitaji mfumo wa kisheria wa utaratibu mpya wa kuomba hifadhi kabla ya kutolewa ufafanuzi.

Halmashauri kuu ya Ulaya yasemaje?

Ursula von der Leyen - Rais wa Halmashauri Kuu ya Umoja wa UlayaPicha: Luis Vieira/AP Photo/picture alliance

Msemaji wa Halmashauri kuu ya Umoja wa Ulaya Adalbert Jahnz, amesema madai ya hifadhi yanaibua maswali ya msingi kuhusu utaratibu wa hifadhi na upatikanaji wa ulinzi.

Chini ya mpango huo wa serikali, watafuta hifadhi hawataweza kuomba moja kwa moja kwenye kituo cha mapokezi kilichoko nje ya Denmark kwasababu hilo linaweza tu kufanyika katika mpaka wa nchi hiyo. Badala yake, watafuta hifadhi wanaofika Denmark watatakiwa kwenda katika taifa la tatu huku maombi yao yakishughulikiwa.

Mnamo mwezi Aprili, serikali ya Denmark ilisema kuwa imetia saini makubaliano na serikali ya Rwanda ambayo hayana msingi wa kisheria lakini yanatoa mwelekeo wa mazungumzo ya siku za baadaye na ushirikiano kati ya mataifa hayo mawili. Gazeti la kila siku la Denmark, Jyllands-Posten, limeripoti kuwa Denmark pia imekuwa katika mazungumzo na Tunisia, Ethiopia na Misri.