1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wapinzani Kongo kufanya maandamano kupinga uchaguzi

23 Desemba 2023

Wagombea watano wa urais kutoka upande wa upinzani nchini Kongo wamesema watafanya maandamano Desemba 27 mwaka huu mjini Kinshasa kupinga ukiukwaji wa taratibu za uchaguzi mkuu uliomalizika.

Dr. Denis Mukwege, Théodore Ngoy and Martin Fayulu
Picha: Paul Lorgerie/DW

Kwa mujibu wa Jean-Marc Kabunda, mwakilishi wa mgombea Martin Fayulu, wanasiasa hao wamewasilisha barua kwa gavana wa jiji la Kinshasa siku ya Jumamosi.

Martin Fayulu mwanasiasa wa Upinzani nchini Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Kongo alipoitembelea DW mjini Bonn 09.11.2022.Picha: Dirke Köpp/DW

Kabunda amesema barua hiyo inaelezea azma ya maandamano hayo ambayo ni ya kupinga ukiukwaji uliojitokeza wakati wa kupiga kura na kabla ya zoezi la kupiga kura na kuongezwa zoezi la kupiga kura kwa siku moja zaidi.

Soma Pia:Kongo yaanza kutangaza matokeo ya awali ya uchaguzi

Mwakilishi wa mgombea Martin Fayulu amesema kasoro zilizotajwa kwenye barua hiyo ni za kutosha kuona kwamba mnamo Desemba 20, 2023, uchaguzi wa nchini Kongo ulikuwa wa udanganyifu.

Tume ya uchaguzi nchini Jamuhuri ya kidemokrasia ya Kongo, CENI, imekiri kuchelewa kuanza shughuli za kupiga kura mnamo Desemba 20 ambapo haikuwezekana kwa baadhi ya vituo kufunguliwa lakini tume hiyo ya uchaguzi imeyakanusha madai ya kufanyika udanganyifu katika uchaguzi huo kwa kuongeza muda wa kupiga kura.

Rais wa Tume huru ya uchaguzi nchini Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (CENI) Denis Kadima.Picha: Giscard Kusema, Presse- und Kommunikationsdienst der Präsidentschaft der Republik Kongo

Katika kikao cha waandishi habari katika mji mkuu Kinshasa, Rais wa CENI Denis Kadima kwa mara nyingine alipinga ukosoaji wa upinzani na waangalizi huru kuwa uchaguzi huo uliorefushwa ulikuwa na vurugu na ulikosa uhalali.

Soma Pia:Kwa nini uchaguzi ni muhimu DR Kongo?

Matokeo ya awali ya uchaguzi wa urais nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo yalianza kutolewa tangu siku ya Ijumaa huku matokeo kamili ya awali ya uchaguzi huo yakiwa yanatarajiwa kutolewa mnamo Desemba 31.

Rais wa DR Kongo kiongozi wa chama cha UDPS kwenye mktano wa kampeni mjini Kinshasa 18/12/2923Picha: AFP

Rais Felix Tshisekedi anayewania muhula wa pili madarakani alikabiliana na wagombea wengine 18 wa upinzani kwenye kinyang'anyiro cha urais. Matokeo ya awali kutoka kwa maelfu ya wapiga kura wa jamii ya Wakongo walioko nje ya nchi yanaonyesha, Rais Felix Tshisekedi anaongoza dhidi ya wapinzani wake.

Matokeo hayo ni kutoka kwa raia wanaoishi Afrika Kusini, Ubelgiji, Ufaransa, Canada na Marekani.

Vyanzo: RTRE/AFP

 

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW