1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wanamgambo wa Taliban wajiimarisha Afghanistan

Isaac Gamba
14 Agosti 2018

Wanamgambo wa Taliban wanadhibiti sehemu kubwa ya kambi ya jeshi kaskazini mwa Afghanistan ambako wamewaua kiasi wanajeshi 10 huku wengine 15 wakijeruhiwa  tangu mapigano yalipoanza upya nchini humo.

Gefechte in Afghanistan
Picha: picture-alliance/AP Photo/M. A. Danishyar

Kwa mujibu wa  Mohammad Tahir Rahmani kiongozi wa ngazi ya juu wa jimbo la Faryadb wanamgambo wa Taliban wamekamata vifaru na silaha kadhaa katika kambi ya jeshi ya Chenayeeha iliyoko  jimbo la Faryab  tangu mapigano yalipoanza tena Jumapili iliyopita.

Anasema hadi sasa vikosi vya serikali havijafanikiwa kuingia katika kambi hiyo ya jeshi na kuwa sehemu kubwa bado iko chini ya udhibiti wa wanamgambo wa Taliban.

Rahman ametaja idadi ya watu waliouawa lakini afisa mmoja wa jimbo nchini humo aliongeza kuwa wanamgambo wa Taliban wamewakamata wanajeshi 40 lakini  hata hivyo wanamgambo 30 wa Taliban  nao pia wameuawa.

Mashambulizi ya wanamgambo wa Taliban kaskazini mwa Afghanistan  yanakuja katika kipindi ambacho mamia  wameuawa pamoja na kujeruhiwa katika jimbo la  Ghazni Kaskazini Magharibi nchini humo lililoko katika barabara kuu  inayounganisha mji wa Kabul na upande wa kusini mwa nchi hiyo.

 Wakazi waliolazimika kuukimbia mji wa Ghazni wanasema wanamgambo wa Taliban wamekata mawasiliano, umeme na huduma za maji huku hospitali zikianza kupungukiwa dawa na maduka  pamoja na majumba kadhaa yakiwemo ya serikali yameharibiwa.

Hayo yanajiri mnamo wakati maafisa wa Afghanistan wakidai vikosi vya usalama  vimewarejesha nyuma  wanamgambo wa Taliban kutoka jimbo la Ghazni na kuwa sasa wanajaribu kuwaondoa kabisa katika maeneo ya pembezoni mwa mji huo.

Nasart Rahimi msemaji wa wizara ya mambo ya ndani  anasema vikosi vya usalama  hapo jana vilikuwa vikiendelea kuwasaka wanamgambo wa Taliban katika kila sehemu walipo huku msemaji wa vyombo vya habari vya kijeshi akisema helikopta za jeshi  zilikuwa zikisaidia katika operesheni  ya ardhini.

Hata hivyo msemaji wa wanamgambo wa Taliban  Zabihullah Mujahdid anakanusha  kuwa wanamgambo hao wameondolewa katika jimbo la Ghazni na kusisitiza mapigano bado yanaendelea.

Umoja wa Mataifa wataka haki za binadamu ziheshimiwe

Mashambulizi ya Taliban katika jimbo la Ghazni nchini AfghanistanPicha: Getty Images/AFP/Z. Hashimi

Wakati huohuo Umoja wa Mataifa unakadiria kuwa zaidi ya raia 100 wameuawa tangu mapambano hayo ya Ghazni yalipoanza Alhamisi iliyopita na kuzitaka pande zinazohusika na mgogoro nchini humo kuheshimu sheria zinazohusiana na haki za binadamu.

Mashambulizi hayo mapya ya  Taliban yanakuja ikiwa ni mwaka mmoja  tangu utawala wa rais wa Marekani Donald Trump ulipoanzisha mkakati wake nchini Afghanistan mnamo wakati wanamgambo wa Taliban  wakiendelea kujiimarisha  katika uwanja wa mapambano  licha ya maafisa wa Marekani kuonesha matumaini ya kupatikana amani nchini humo.

Hatua hii inazidi kuibua maswali juu ya  uwezekano wa Marekani wa kukomesha mapigano nchini  Afghanistan.

 Wizara ya ulinzi ya Marekani Pentagon imetangaza Jumatatu wiki hii kuwa afisa wa kijeshi wa nchi hiyo  Reymond Rarogal  mwenye umri wa miaka 36 amefariki Jumapili iliyopita  kufuatia majeraha aliyoyapata wakati wa operesheni iliyofanyika katika jimbo la Helmand.

Kutokana na kurejea tena kwa mashambulizi ya kundi la Taliban nchini Afghanistan baadhi wanahoji iwapo  Rais Trump  atafikia hatua ya kushindwa   kujihusisha kijeshi nchini humo  ambapo Marekani inatumia dola bilioni 4 kwa mwaka  ili kuviongezea nguvu kijeshi vikosi vya Afghanistan.

Mwandishi: Isaac Gamba/APE/RTRE

Mhariri: Bruce Amani

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW