1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaMsumbiji

Wananchi wa Msumbiji wanapiga kura katika uchaguzi mkuu

9 Oktoba 2024

Wananchi wa Msumbiji wanapiga kura Jumatano (09.10.2024) katika uchaguzi ambao huenda ukakirejesha madarakani chama tawala cha Frelimo na kuendelea kutawala kwa nusu karne.

Wananchi wa Msumbiji wanapiga kura katika chaguzi tatu
Wananchi wa Msumbiji wanapiga kura katika chaguzi tatuPicha: Alfredo Zuniga/AFP/Getty Images

Takribani wapiga kura milioni 17 katika taifa hilo lenye watu milioni 31, wamejiandikisha kupiga kura kumchagua rais ajaye, pamoja na wabunge 250 na magavana wa majimbo.

Vituo vya kupigia kura vilifunguliwa saa moja asubuhi kwa saa za Msumbiji na vitafungwa saa 12 jioni. Wagombea wanne wanashindana katika uchaguzi huo kuchukua nafasi ya Rais Filipe Nyusi, ambaye amemaliza muda wake wa mihula miwili kwa mujibu wa katiba.

Mgombea anayepewa nafasi kubwa ya kushinda ni Daniel Chapo, wa chama cha Frelimo mwenye umri wamiaka 47. Wapinzani wa Chapo ni Venancio Mondlane, anayesimama kama mgombea binafsi, aliyekuwa kamanda wa waasi, Ossufo Momade, na kiongozi wa chama kidogo cha upinzani, Lutero Simango. Matokeo yanatarajiwa kutolewa katika muda wa wiki mbili zijazo.