1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tuzo ya Nobeli ya Tiba 2024 yaenda Marekani

7 Oktoba 2024

Wanasayansi wa Marekani Viktor Ambros na Gary Ruvkun wameshinda tuzo ya Nobeli ya masuala ya tiba ya mwaka 2024, kwa ugunduzi wao wa MicroRNA kuhusu kukua na kuishi kwa seli za viumbe hai.

Tuzo ya nobeli ya masuala ya Tiba 2024 Gary Ruvkun na Forscher Victor Ambros
Washindi wa Tuzo ya Nobeli ya masuala ya Tiba 2024, Viktor Ambros na Gary Ruvkun Picha: Mass General,UMass/AP/dpa/picture alliance

Katibu Mkuu wa Kamati ya taasisi ya tuzo ya Nobeli ya Karolinska iliyoko Stockholm, Sweden Thomas Perlmann, amewatangaza wanasayansi hao kuwa washindi wa tuzo hiyo ya masuala ya fiziolojia au tiba. Kazi yao ilisaidia kuelezea namna seli zinavyotofautiana katika ukuaji wake kama zile za misuli na neva, japokuwa seli hizo kwa wanadamu zote ziko sawa katika kukua kwake na kuishi.

Tasisi inayosimamia tuzo ya Nobel, imesema katika taarifa yake kwamba washindi hao wamegundua aina mpya ya chembechembe ndogo ambazo zina jukumu muhimu katika udhibiti wa jeni. Ugunduzi wa maprofesa hao utaongeza uelewa zaidi wa magonjwa kama vile kifafa.

Akizungumza na shirika la habari la Reuters, Amros amesema teknolojia mambo leo ya mRNA ni mtandao wa mawasiliano miongoni mwa jeni, inayowezesha seli ndani ya miili ya binaadamu kutoa aina tofauti ya mifumo ya ufanyaji kazi. Na hii ndiyo sababu kwamba seli zina sifa ya kuwa tofauti, kwa mfano seli za misuli na neva, ingawa zinafanana.

Chanjo za mRNA zilitumika pakubwa katika kupambana na maambukizi zaidi ya virusi vya UVIKO-19 ulimwenguni

Wakati udhibiti wa jeni unapovurugika, hali hiyo inaweza kusababisha magonjwa makubwa kama saratani, kisukari au kuathiri kinga mwilini. Kuelewa kanuni ya jinsi jeni zinavyofanya kazi imekuwa lengo muhimu kwa wanasayansi katika kipindi cha miongo mingi. Wanasayansi kwa muda mrefu wamezingatia kuwa ni muhimu zaidi kuzifafanua kanuni utendajikazi wa jeni.

Washindi hao wa tuzo ya tiba Victor Ambros mwenye umri wa miaka 71, Profesa katika chuo kikuu cha matibabu cha Massa-chu-setts na mwenzake Gary Ruvku mwenye umri wa miaka 72, profesa katika chuo kikuu cha matibabu cha Harvard wataopokea jumla ya dola za kimarekani milioni 1.1.

afp/ap