1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wanawake Zimbabwe wapambana dhidi ya ubaguzi wa kijinsia

8 Machi 2021

Kuna madereva wachache wa kike wa malori makubwa nchini Zimbabwe, lakini Molly Manatse hapendi kuangaziwa kwa jinsia yake. Kwenye karatasi, Zimbabwe ina sheria zinazohakikisha haki za wanawake. Lakini hazitekelezwi.

Simbabwe  Nahrungsmittelknappheit
Picha: picture-alliance/AP Photo/T. Mukwazhi

"Kwangu imejulikana wakati wote kama kazi ya wanaume, lakini sisemi kwamba mimi ni dereva mwanamke. Sisi ni madereva tu, tunafanya kazi sawa," anasisitiza Manatse mwenye umri wa miaka 31, dereva wa lori kutoka Zimbabwe ambaye kipato chake kinamsaidia kuwahudumia ndugu zake waliopoteza ajira zao kutokana na covid-19.

Kuanzia kuendesha malori na kutengeneza magari hadi kuwapa moyo wasichana wanaoishi na ulemavu kutafuta nafasi zao katika jamii, wanawake nchini Zimbabwe wanakataa kufasiriwa kwa jinsia zao au mazingira, hata wakati janga likiwaathiri vikali zaidi na kuwawekea mzigo zaidi.

Soma zaidi: Wanawake Zimbabwe wataka usawa wa kijinsia

Wakati siku ya kimataifa ya wanawake ikiadhimishwa kote dunia siku ya Jumatatu, wanawake nchini Zimbabwe wanasherehekea mafanikio walioyapata katika kukabiliana na ubaguzi katika maeneo ya kazi na wanakiri kwamba juhudi zaidi zinahitajika.

Katika matukio mengi, wanawake wa Zimbabwe wamekuwa viongozi kulisaidia taifa hilo la kusini mwa Afrika lenxe matatizo kukabiliana na madhara pacha ya athari za janga la Covid-19 na mporomoko unaoendelea wa kiuchumi.

Hata hivyo, wanawake wengi wanasema siyo rahisi kuapta usawa au utambuzi wa kitaaluma na mara nyingi wanakumbushwa juu ya jukumu la kijadi la wanawake nchini Zimbabwe.

Wanawake wa zimbawe wakiwa katika shamba la tumbaku.Picha: picture-alliance/Chad Ehlers

"Unaporudi nyumbani wanakutarajia upike, wanakutarajia ufue nguo. Kazi zote za nyumbani, unapaswa kuzifanya. Hiyo ni changamoto," Manatse aliliambia shirika la habari la Associated Press, wakati akijiandaa kwa ajili ya safari yake ya kilomita 1,700 kuelekea mji wa bandari wa Durban katika nchi jirani ya Afrika Kusini. Ndiye dereva pekee wa kike katika kampuni ya malori inayowaajiri madereva 80, alisema.

Memory Mukabeta, mwenye umri wa miaka 37, anaendesha duka la kutengeneza magari, kazi ambayo kawaida inatazamwa kuwa makshusi kwa wanaume. Kama ilivyo kwa Manatse, siku hizi anasaidia kuwasaidia wanachama wa familia yake kubwa ambao maisha yao yameathiriwa na vizuwizi vilivyosababishwa na sheria la kudhibiti kuenea kwa virusi vya corona.

Soma pia: Wanawake Zimbabwe waanadamana

Kwenye karatasi, Zimbabwe ina sheria zinazohakikisha haki za za wanawake katika maeneo ya kazi na nyumbani. Nchi hiyo ilisaini mikataba ya kimataifa inayounga mkono usawa wa kijinsia.

Lakini ukosefu wa utekelezaji, pamoja vitendo vya mafunzo ya kitamaduni vinavyoimarisha ukosefu wa usawa vinamaanisha wanawake, wanaochangia asilimia 52 ya wakaazi milioni 15 wa taifa hilo, bado wanasalia nyuma katika elimu, afya na kazi, kwa mujibu wa shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia watoto.

Shirika la wanawake la Umoja wa Mataifa, UN Women, linakadiria kuwa wanawake milioni nane kuliko wanaume watatumbukia katika umaskini mkubwa katika eneo la Afrika Kusini mwa jangwa la Sahara mnamo mwaka 2021 kutokana na janga la Covid-19.

Ingawa janga limewaathiri zaidi wanawake, badala ya kulalamika wanaonesha ujasiri wao," alisema Florence Mudzingwa, ambaye shirika lake la Hope Resurrect Trust, linawapa wasichana wanaoishi na ulemavu, ujuzi, vifaa na imani kutafuta njia yao katika ulimwengu, licha ya jinsia yao na ulemavu.

Chanzo: APE

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW