Wangapi watakufa?: Ugonjwa wa ajabu unaoua tembo Kenya
21 Agosti 2026
Tembo wanakufa mmoja baada ya mwingine kusini mwa Kenya kutokana na tatizo la kiafya ambalo chanzo chake bado hakijafahamika. Vifo hivyo vimezua hofu katika jamii zinazowazunguka wanyama hao, huku wataalamu wakitofautiana kuhusu ikiwa ni ugonjwa au sumu inayotumiwa mashambani.
Tembo wa hivi karibuni kufa ni dume mwenye umri wa miaka 11 aliyeitwa Genghis Khan. Alikutwa akiwa amelala chini, akirusha vumbi huku akijaribu bila mafanikio kusimama.
Madaktari wa mifugo walimpa sindano ya glukosi, lakini hali yake iliendelea kuwa mbaya. Alikuwa akipumua kwa shida na hatimaye alikufa Jumanne.
Tangu mwezi Juni, takribani tembo 20 wamekufa nchini Kenya, wengi wao wakiwa majike na madume madogo. Wanyama wote waliokufa wameonyesha dalili zinazofanana, zikiwemo kupooza kwa sehemu ya mwili, kushindwa kusimama na kupumua kwa shida.
Vifo hivyo vimeripotiwa katika mfumo wa ikolojia wa Amboseli, eneo maarufu kwa makundi makubwa ya tembo na mandhari ya Mlima Kilimanjaro ulioko nchini Tanzania. Amboseli ni moja ya maeneo muhimu ya utalii nchini Kenya.
Tembo wanateseka kwa siku kadhaa
Patrick Papatiti, mkuu wa operesheni katika ardhi ya jamii ya Olgulului, amesema baadhi ya tembo huteseka kwa muda mrefu kabla ya kufa.
"Unamkuta mmoja akihangaika kwa siku moja, siku mbili au hata siku tatu, mpaka anapokufa kabisa,” amesema Papatiti. Eneo analolisimamia linajumuisha hifadhi ya Kitenden B, ambako Genghis Khan alipatikana.
Mwishoni mwa Julai, Shirika la Huduma za Wanyamapori la Kenya, KWS, lilisema vipimo vya sumu vilibaini kiwango kikubwa cha sianidi katika mizoga ya tembo. Matokeo hayo ya awali yaliibua dhana kwamba huenda wanyama hao walikula mimea au mazao yenye dawa kutoka mashamba ya jirani.
Hata hivyo, baadhi ya wasimamizi wa wanyamapori, wahifadhi na wakazi wa eneo hilo wanapinga maelezo hayo. Wanasema hakuna ushahidi wa kutosha kuthibitisha kwamba tembo hao wamekufa kutokana na sumu.
Papatiti, ambaye amezaliwa na kukulia katika jamii ya Wamaasai, anaamini chanzo kinaweza kuwa ugonjwa unaowaathiri tembo pekee. Anasema kama sianidi ingekuwa sababu, wanyama wengine wanaokula mizoga hiyo pia wangekufa.
Nzi, fisi na tai wameonekana wakila mizoga ya tembo bila kuonyesha dalili za kuathiriwa. Hilo limeongeza mashaka kuhusu nadharia ya sumu.
Joel Nyika, msimamizi wa mfumo wa ikolojia wa Amboseli katika serikali ya Kaunti ya Kajiado, anasema hali hiyo haifanani na visa vya kawaida vya sumu.
"Ikiwa mnyama mwingine anakula mzoga huo na hafi, basi ni wazi kwamba chanzo hakiwezi kuwa kemikali,” amesema Nyika.
KWS yakataa uwezekano wa ugonjwa wa kuambukiza
Nyika pia ametilia shaka uwezekano kwamba sianidi hiyo ilitokana na aina fulani ya mimea. Kwa mujibu wake, kama mimea ya eneo hilo ndiyo yenye sumu, mifugo inayolishwa karibu na maeneo hayo pia ingeathirika.
"Kwa mtazamo wetu kama wasimamizi wa wanyamapori, tunaamini huenda ni ugonjwa unaowaathiri tembo hawa pekee,” amesema.
Hata hivyo, KWS ilisema Agosti 7 kwamba matokeo yaliyopatikana hadi wakati huo hayakuonyesha kuwapo kwa ugonjwa wa kuambukiza kutoka kwa mnyama mmoja kwenda kwa mwingine. Shirika hilo pia liliwahakikishia watalii kwamba wanaweza kuendelea kutembelea eneo hilo.
Lakini hali inayoonekana kwenye hifadhi za eneo hilo imezidi kuongeza wasiwasi. Waandishi wa habari wa shirika la AFP waliona mizoga sita katika siku moja ndani ya hifadhi ya Kimana. Baadhi ilikuwa mipya na mingine ilikuwa imekaa kwa muda.
Askari wa hifadhi pia waliona tembo walioathirika wakipooza sehemu ya miili yao na kushindwa kusimama. Hata hivyo, walisema hawakuwa na ruhusa ya kuzungumza hadharani kuhusu hali hiyo.
Wakulima wakataa lawama
Baadhi ya wakulima Wamaasai wanaoishi karibu na hifadhi hizo pia wanakataa madai kwamba mazao yao yanaweza kuwa chanzo cha vifo. Wanasema wao pamoja na mifugo yao hutumia chakula na maji kutoka mazingira hayo bila kuathirika.
Noah Saatia, mkulima mwenye umri wa miaka 52, amesema jamii za eneo hilo zina uhusiano mkubwa na tembo na zinaumia kuwaona wakifa.
"Wanapokufa, inauma sana. Hatujui sababu ya vifo vyao, lakini tuna uhakika hawafi kwa sababu ya chakula,” amesema Saatia akiwa katika shamba lake la mahindi lililozungushiwa uzio ili kuzuia wanyama kuingia.
Baadhi ya mizoga iliyopatikana inaonyesha ukubwa wa janga hilo. Mtoto wa tembo mwenye umri wa miezi minne alikutwa akiwa ameliwa sehemu ya mwili na fisi, huku nzi wakizunguka mabaki yake.
Katika eneo jingine, tai kadhaa walikuwa wakila mzoga wa tembo jike aliyekuwa karibu kujifungua. Mtoto wake ambaye hakuzaliwa pia alikufa.
"Ni tembo wangapi watakufa?”
Paula Kahumbu, mhifadhi na mkuu wa shirika la Wildlife Direct, amesema ushahidi unaounga mkono nadharia ya dawa za kuua wadudu bado hautoshi.
Amehoji kwa nini ni madume machache makubwa yaliyokufa, wakati kundi hilo ndilo linalojulikana zaidi kwa kuvamia mashamba na hivyo kuwa na uwezekano mkubwa wa kula mazao yenye dawa.
Papatiti pia amekataa dhana kwamba tembo hao waliwekewa sumu kwa makusudi. Kwa maoni yake, mjadala haupaswi kulenga kutafuta watu wa kulaumiwa kabla ya chanzo halisi cha vifo kuthibitishwa.
Mashirika kadhaa ya mazingira yamekuwa yaangalifu kuzungumzia suala hilo na baadhi yamekataa kutoa maoni zaidi ya kutoa wito wa uchunguzi wa kina.
Papatiti anaamini idadi halisi ya tembo waliokufa inaweza kuwa kubwa kuliko takwimu zilizotangazwa. Pia ana hofu kwamba tatizo hilo huenda limeanza kuwaathiri tembo wanaovuka mpaka na kuingia Tanzania.
Kwa sasa hakuna jibu la wazi kuhusu chanzo cha vifo hivyo wala namna ya kuzuia tembo wengine kuathirika. Hali hiyo imemfanya Papatiti kuuliza: "Ni tembo wangapi watakufa kabla hatujaweza kukomesha hili?”