1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Vikosi vya Israel vyawauwa watu watatu Ukingo wa Magharibi

Angela Mdungu
30 Januari 2024

Vikosi vya Israel vimewauwa wanamgambo watatu wa Kipalestina katika msako mkali uliofanyika kwenye hospitali katika Ukingo wa Magharibi. Ghasia zimekuwa zikiongezeka kwenye eneo hilo tangu vita vilipoanza.

Ukanda wa Gaza | Gari la wagonjwa katikati ya magari ya jeshi la Israel.
Gari la wagonjwa likipita katikati ya magari ya vikosi vya Israel, GazaPicha: Nasser Nasser/AP Photo/picture alliance

Hayo yanajiri wakati jeshi la Israel likijiandaa kuwahamisha baadhi ya wanajeshi wake kutoka Gaza kuelekea katika eneo la mpaka wake na Lebanon.

Jeshi la Israel limesema kuwa vikosi vyake viliingia katika hospitali ya Ibn Sina kaskazini mwa mji wa Jenin katika Ukingo wa Magharibi, mapema Jumapili walikowafyatulia risasi na kuwauwa wanaume watatu ambao Hamas imedai kuwa ni wanachama wake.

Lilifafanua kuwa, walengwa wa operesheni hiyo iliyofanyika usiku kucha ilikuwa dhidi ya mwanachama mmoja wa kundi la Hamas na Wapalestina wengine wawili ambao ni wafuasi wa itikadi kali za Kiislamu.

Soma zaidi: Machafuko yaongezeka Ukingo wa Magharibi

Jeshi hilo limesema wanaume hao walikuwa wakiitumia hospitali ya Ibn Sina kama eneo la maficho yao na kuwa angalau mtu mmoja alikuwa akipanga kufanya mashambulizi.

Kwa upande wake Wizara ya afya ya Palestina imesema kuwa, wanajeshi wa Israel walifyatua risasi ndani ya wodi za hospitali hiyo na imeitaka Jumuiya ya kimataifa iizuie Israel kufanya operesheni zake katika hospitali.

Wizara hiyo imesema kuwa hadi sasa Wapalestina 366 wameuwawa katika Ukingo wa Magharibi pekee tangu kuanza kwa vita.

Vikosi vya ardhini vya Israeli vimekuwa pia vikifanya operesheni zake katika mji wa Khan Younis, ambao ni mji wa kiongozi wa kundi la Hamas Yahya Sinwar ambapo shirika la hilali nyekundu la Palestina liliripoti mashambulizi kuizunguka hospitali ya Al Amal usiku kucha.

Israel yajiandaa kuvihamishia mpakani mwa Lebanon baadhi ya vikosi vyake

Katika hatua nyingine, jeshi la Israel liliarifu kuwa lilikuwa likijiandaa kuvihamisha baadhi ya vikosi vyake kutoka kwenye Ukanda wa Gaza kuelekea kwenye mpaka wa Lebanon.

Ni  wakati wasuluhishi wa kimataifa wakifanya juhudi za kupata makubaliano mapya ili jeshi hilo lisitishe vita vyake na Hamas huku wakaazi wa Gaza wakikabiliwa na mgogoro mbaya wa kiutu.

Wakaazi wa Gaza wanaokabiliwa na uhaba wa mahitaji muhimuPicha: Abed Rahim Khatib/Anadolu/picture alliance

Licha ya hali hiyo ngumu, baadhi ya mataifa yamesitisha ufadhili wake kwa Shirika la Umoja wa Mataifa linalowahudumia Wapalestina UNRWA kutokana na tuhuma kuwa, wafanyakazi wake 12, kati ya waajiriwa wote 13,000 wa shirika hilo ndani ya Gaza, walihusika katika shambulio la Oktoba 7 lililofanywa na kundi la Hamas dhidi ya Israel.

Hayo yanajiri wakati Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa akitazamiwa kukutana na mataifa ambayo ni wafadhili muhimu yaliyositisha misaada kwa shirika hilo linalowahudumia wakimbizi wa Kipalestina.

 

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW