Wapatanishi wa Afrika washindwa kumshawishi Gbagbo aachie madaraka
4 Januari 2011Wapatanishi wa Kiafrika wameondoka Cote d'Ivoire bila ya hiyo jana kufanikiwa kumshinikiza Laurent Gbagbo kumkabidhi madaraka mpinzani wake Alassane Ouattara. Viongozi hao leo watakutana na Rais wa Nigeria Goodluck Jonathan aliye pia mwenyekiti wa hivi sasa wa jumuiya ya kiuchumi ya nchi za Afrika ya Magharibi, ECOWAS. Marais wa Benin, Sierra Leone na Cape Verde, wakiiwakilisha ECOWAS na Waziri mkuu wa Kenya, Raila Odinga, kwa niaba ya Umoja wa Afrika walikwenda Cote d'Ivoire ambako walikuwa na mazungumzo pamoja na Gbagbo kabla ya kuonana na Ouattara.
ECOWAS imetishia kutumia nguvu za kijeshi ikiwa Gbagbo atakataa kumkabidhi madaraka Ouattara anayetambuliwa na jumuiya ya kimataifa kuwa ni mshindi wa uchaguzi uliofanyika mwezi wa Novemba. Kwa mujibu wa ripoti za vyombo vya habari, Gbagbo ameahidiwa na viongozi hao wa Kiafrika usalama wake na kwamba hatoshtakiwa ikiwa ataondoka kwa amani.
Mwandishi: Prema Martin/RTRE
Mhariri: Josephat Charo