Wapatanishi wa Israel na Hamas wazungumza Cairo
5 Oktoba 2025
Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu ameelezea matumaini ya mateka kuachiliwa ndani ya siku chache zijazo.
Msukumo huu mpya wa kidiplomasia unafuatia hatua ya kundi la Hamas kutangaza kukubaliana na mpango wa amani wa rais Donald Trump wa Marekani unaojumuisha kuachiliwa huru kwa mateka wa Israel pamoja na mamia ya Wapalestina wanaoshikiliwa katika jela za Israel. Ikulu ya White House imesema kuwa Trump ametuma wajumbe wawili nchini Misri ambao ni mkwe wake Jared Kushner na mjumbe wa Mashariki ya Kati Steve Witkoff.
Vyombo vya habari vyenye mafungamano na serikali ya Misri vimesema pande zinazozozana zitafanya mazungumzo yasiyo ya moja kwa moja leo na kesho Jumatatu, kabla ya tarehe ya kuadhimisha mwaka wa pili wa shambulio la Oktoba 7 la Hamas ambalo lilisababisha kuzuka kwa vita hivi. Licha ya miito ya Trump, Israel hata hivyo imeendeleza mashambulizi yake katika Ukanda wa Gaza.