Wasomali kupelekewa msaada wa chakula kwa ndege kuanzia leo!
27 Julai 2011Maafisa wa Shirika la Chakula Duniani la Umoja wa Mataifa, WFP wamesema wanatumai kwamba kazi ya kupeleka misaada mjini Mogadishu kwa ndege, itaanza leo baada ya kuchelewa kutokana na sababu za kiurasimu nchini Kenya. Msaada huo ni pamoja na chakula kilichotiwa lishe nzito kwa ajili ya idadi kubwa ya watu waliomo katika hatari ya kufa njaa kwenye eneo la Pembe ya Afrika.
Janga la njaa katika eneo hilo limesababishwa na ukame mbaya usiokuwa na mithili katika kipindi cha miaka 60 iliyopita. Kwa mujibu wa taarifa maalfu ya watu wanaikimbia Somalia ili kutafuta chakula na maji kwingineko
Juhudi za mashirika ya misaada za kuwapelekea watu chakula na mahitaji mengine zinazuiwa na wapiganaji wa kundi la waislamu wenye itikadi kali- al Shabaab. Maeneo ya kati na ya kusini mwa Somalia yanadhibitiwa na kundi la watu hao.
Umoja wa Mataifa umesema Wasomali zaidi ya milioni tatu na nusu sasa wamo katika hatari ya kufa njaa. Maalfu tayari wamekimbilia Kenya na maalfu wengine wanatarijiwa kuwasili nchini humo.