Watetezi wa haki wataka Polepole arejeshwe akiwa hai
7 Oktoba 2025
Jeshi la Polisi Oktoba 7 pamoja na kusisitiza kuwa limeanza uchunguzi kuhusu kupotea kwa mwanasiasa Humphrey Polepole limesema linamtafuta ndugu wa Polepole, Augustino Polepole ili alisaidie jeshi hilo kuthibitisha shutuma alizotoa kuwa afisa wa Jeshi la Polisi alihusika katika tukio la utekwaji wa Humphrey Polepole.
Asasi za kiraia nazo zimeibuka na kuzitaka mamlaka hasa Jeshi la Polisi kuchukua hatua za haraka kuchunguza tukio hilo. Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu(LHRC) kimesema iwapo Polepole anashikiliwa kwa tuhuma zozote basi mamlaka hazina budi kumfikisha mahakamani ili haki itendeke kwa mujibu wa sheria.
Wakili wa Polepole aiandikia mahakama
Wakili Peter Kibatala ameaindikia mahakama ombi maalum kuitaka mahahama hiyo itowe amri ya dharura ya kutaka serikali kumpeleka Polepole mahakamani na ama kutoa sababu za kisheria za kumshikilia au Habas Corpus. Kibatala aliiandikia mahakama amri hiyo jana Oktoba 6 akieleza kuwa anazitaka mamlaka za raia kutoa taarifa juu ya usalama na maslahi ya kisheria ya Balozi Humphrey Polepole ambaye wakili huyo alimtambulisha kama mteja wake.
Uongozi wa CCM ambako Polepole amekuwa akisisitiza kuwa yeye bado ni mwanachama haukupatikana kuzungumzia sakata la kutoweka kwa mwanachama wao.
Siku ya Jumanne Tanzania iliamka na taarifa za kutekwa kwa mwanasiasa na aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Cuba ambaye pia alikuwa akisimamia visiwa vya Karibiani, Amerika ya Kati, Columbia na Guetemala. Polepole ambaye baada ya kujiuzulu wadhifa wake wa ubalozi Julai mwaka huu aligeuka kuwa mkosoaji mkubwa wa serikali ya CCM, amewahi pia kuwa Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Mkuu wa Wilaya na Mbunge kwa nyakati tofauti.