1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Watoto milioni 72 watumikishwa Afrika

12 Juni 2019

Mtoto mmoja katika kila watano, sawa na milioni 72.1, anafanyishwa kazi kwenye mataifa ya Afrika yaliyo kusini mwa Jangwa la Sahara, ambapo nusu yao wakiwa chini ya umri wa miaka 11.

Ghana Junger Mann in der Zabzugu-Tatale Region
Ajira nyingi za watoto hazitajwi na wala hazina mishahara maana hufanywa kwa ajili ya familia.Picha: Imago/D. Delimont

"Nilianza kazi hii miaka minne iliyopita kwenye familia mbalimbali. Kawaida nilikuwa sipewi chakula cha kutosha na waajiri wangu walikuwa wakinidhalilisha", anasema Fatoumata ambaye ndio kwanza alikuwa na umri wa miaka 12 tu alipoondoka kijijini kwake nchini Mali kusaka kazi mjini.

Kwa wazazi wake, elimu haikuwa kipaumbele, badala yake akawa analazimika kuamka mapema alfajiri kuihudumia familia ngeni, kuandaa kistaftahi chao na kuwapeleka watoto wao skuli. Yaani kazi ya mzazi, baba au mama, inafanywa sasa na mtoto mdogo, mtumishi wa nyumbani.

Akiwa sasa na umri wa miaka 16, Fatoumata anaonekana mkubwa zaidi kuliko umri wake halisi, maana ameshapitia mengi na mwingi. "Ili kupokea mshahara wangu wa faranga 10,000, nililazimika kuvumilia machungu yote ya dunia na, hata hivyo, wakati mwengine nilirejea kwa wazazi wangu kijijini nikiwa mikono mitupu," anasema msichana huyo.

Lakini Fatoumata si pekee. Duniani kote, watoto wanalazimishwa kufanya kazi za hatari zinazoyaweka rehani maisha yao, usalama na ukuwaji wao wa kimaadili.

Idadi ya watoto wanaofanyishwa kazi ni kubwa zaidi kwenye mataifa ya Afrika yaliyo kusini mwa Jangwa la Sahara kuliko kwengineko duniani. 
Mtoto mmoja kwa kila watano, yaani watoto milioni 72.1, na nusu yao wakiwa chini ya umri wa miaka 11, ni wahanga wa jaala hii.

Ajira nyingi za watoto hazitajwi na wala hazina mishahara maana hufanywa kwa ajili ya familia.Picha: picture-alliance/Photoshot/Xinhua/R. Alizadah

Hii inawafanya watoto wa Kiafrika kuwa ndio watumikishwao wakiwa wadogo zaidi duniani.

Kutumikishwa kwenye ukahaba

"Utumikishwaji watoto una sura nyingi, si moja," anasema Ninja Charbonneau wa Shirika la Watoto la Umoja wa Mataifa (UNICEF).

"Ajira za kulazimishwa, ukahaba na kufanyishwa kazi migodini ni baadhi yao. Na madhara yanayowapata watoto kwa kazi hizi ni makubwa sana. Huwa hawawezi kukuwa kama wakuwavyo wenzao wengine, ikimaanisha kuwa huwa hawaendi skuli, na hapo mduara wa papo kwa papo wa maovu na umasikini ndipo unapoanzia," anaongeza.

Watoto wengi barani Afrika hufanyishwa kazi kwenye kilimo na ufugaji, wengine wapatao milioni nane wakifanya kazi za utumwa wa majumbani kama alivyo Fatoumata, na wengine milioni tatu wakiwa viwandani.

Lakini kawaida ajira nyingi za watoto huwa hazitajwi na wala hazina mshahara, maana wengi wao huzifanyia kwenye familia zao.

Silja Fröhlich/Mahamadou Kane 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW