1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
UhamiajiUgiriki

Watu 15 wafa baada ya boti kugongana

4 Februari 2026

Mamlaka nchini Ugiriki zinasema watu 15 wamekufa kufuatia ajali ya kugongana kwa mashua ya walinzi wa pwani ya Ugiriki na ile ya wahamiaji kando ya ufukwe wa Kisiwa cha Chios siku ya Jumanne (Februari 3).

Ugiriki Chios 2026 | Shughuli za uokozi baada ya meli kugongana na boti ya wahamiaji
Maafisa wa walinzi wa pwani wa Ugiriki wakifanya shughuli za uokozi kwenye kisiwa cha Chios mashariki mwa Bahari ya Aegean baada ya watu kadhaa kufariki kwenye ajali ya mgongano wa boti ya mwendo kasi iliyokuwa imewabeba wahamiaji na boti ya doria ya walinzi wa pwani.Picha: Pantelis Fykaris/Politischios.gr/dpa/picture alliance

Naibu Meya wa kisiwa hicho, Pantelis Vroulis, aliiambia televisheni ya umma, ERT, kwamba miili 15 ndiyo iliyoopolewa na yote ilikuwa ya wahamiaji.

Televisheni hiyo ilitangaza kuwa watu 25 walikuwa wamepelekwa kwenye hospitali ya kisiwa hicho, 11 wakiwa watoto wadogo na wawili wakiwa maafisa wa kikosi cha ulinzi wa pwani.

Vyombo vya habari vinasema watu kadhaa walikuwamo kwenye mashua hiyo ya wahamiaji iliyokuwa ikitokea Uturuki kuelekea Kisiwa cha Chios.

Kwa mujibu wa Shirika la Wakimbizi la Umoja wa Mataifa, UNHCR kiasi cha wahamiaji 1,000 wameingia kwenye visiwa vinavyotawaliwa na Ugiriki kwenye Bahari ya Aegan wakitokea Uturuki tangu mwanzoni mwa mwaka huu.

Shada la maua linaelea kwenye Bahari ya Mediterania, baada ya watu kumaliza maandamano kwenye ufuo katika eneo la ajali ya meli mnamo Machi 11, 2023 huko Steccato di Cutro, mkoa wa Calabria, kusini mwa ItaliaPicha: Gianluca Chininea/AFP/Getty Images

Sababu za ajali yatajwa

Ajali hiyo ilitokea baada ya mashua ya Walinzi wa Pwani kujaribu kuikamata boti ya wahamiaji na kuilazimisha kugeuza njia. Kulingana na taarifa ya Walinzi wa Pwani, "Nahodha wa boti hiyo ya mwendo kasi ambayo haikuwa na taa za kuiongoza na aliyewabeba abiria wa kigeni alikataa kuheshimu ishara za maonyo zilizotolewa na Walinzi wa Pwani."

Badala yake, nahodha huyo aligeuza boti hiyo na kisha kugongana na upande wa boti ya doria ya Walinzi wa Pwani," imesema taarifa hiyo na kuongeza kuwa "mgongano ndio ulisababisha boti hiyo kupinduka na kuzama."

Wahamiaji 4 wamefariki, 29 wapotelea baharini nchini Uhispania

01:09

This browser does not support the video element.

Idadi kubwa ya wahamiaji bado wanazama ama kupotea baharini

Idadi kubwa ya wahamiaji huvuka Bahari ya Mediterania kila mwaka wakijaribu kuingia Ulaya. Shirika la Wakimbizi la Umoja wa Mataifa lilisema mwezi Novemba kwamba zaidi ya watu 1,700 walikufa ama kupotea mwaka 2025 kwenye njia mbalimbali zinazotumiwa na wahamiaji kwenda Ulaya katika Bahari ya Mediterania na katika Bahari ya Atlantiki pembezoni mwa pwani ya Afrika magharibi.

Na kulingana na Shirika la Wahamiaji ulimwenguni, IOM, karibu wahamiaji 33,000 wamekufa ama kupotea kwenye Bahari ya Mediterania tangu 2014.

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW