Watu 64 wauawa katika ghasia za mjini Rio de Janeiro
29 Oktoba 2025
Watu 64 wameuawa katika makabiliano ya mjini Rio de Janeiro nchini Brazil, baada ya polisi kuanzisha msako mkubwa zaidi kuwahi kutokea dhidi ya magenge ya dawa za kulevya.
Takriban maafisa 2,500 waliokuwa na silaha nzito, wakisaidiwa na magari ya kivita, helikopta na ndege zisizo na rubani walishiriki katika operesheni hiyo, iliyolilenga genge kuu la ulanguzi wa dawa za kulevya nchini Brazil katika vitongoji viwili maskini, kaskazini mwa Rio.
Milio ya risasi ilisikika katika maeneo ya karibu na uwanja wa kimataifa wa ndege huku moshi mzito ukifuka kutokana na milipuko kadhaa.
Wakaazi walihangaika kutafuta mahali pa kujificha na maduka yakifunga milango yake. Serikali kuu ya Brazil imesema msako huo ulilenga kukomesha genge moja linaloitwa Comando Vermelho.