1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waziri mkongwe wa Tanzania William Lukuvi afariki dunia

25 Machi 2026

Rais wa Tanzania, Samiam Suluhu Hassan, ametuma salamu za rambirambi kufuatia kifo cha mbunge wa Isimani na Waziri wa nchi, Ofisi ya Rais, Sera, Uratibu, Bunge na Walemavu, William Lukuvi.

Lukuvi amehudumu kama mbunge kwa zaidi ya miongo mitatu
Marehemu William Lukuvi amehudumu kama mbunge kwa zaidi ya miongo mitatuPicha: Stringer/REUTERS

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samiam Suluhu Hassan, wadau wa siasa, wabunge na viongozi katika kada mbalimbali hapa nchini, wametuma salamu za rambirambi kufuatia kifo cha mbunge wa Isimani na Waziri wa nchi, Ofisi ya Rais, Sera, Uratibu, Bunge na Walemavu, William Lukuvi.

Lukuvi amefariki dunia kwa mshtuko wa moyo. Lukuvi atakumbukwa kama miongoni mwa viongozi waliohudumu bungeni kwa miongo zaidi ya mitatu.

Taifa la Tanzania limeamshwa na msiba mzito wa Mbunge wa Isimani, William Vangimembe Lukuvi, anayetajwa kama miongoni mwa viongozi wenye ushawishi mkubwa serikalini na waliohudumu katika bunge tangu kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi Tanzania mwaka 1995.

Salamu za rambirambi za Rais Samia Suluhu Hassan

Rais Samia Suluhu Hassan,ametuma salamu zake za rambirambi kupitia ukurasa wake wa X, akimtaja Lukuvi kama kiongozi  mwenye uzoefu, mzalendo na mtumishi wa umma aliyelitumikia Taifa  kwa uadilifu, weledi na kujitolea.

Rais Samia atoa salamu za rambirambi kwa kifo cha LukuviPicha: Tanzania State House

Viongozi wa CCM, nao wamemzungumzia, Lukuvi kama mwadilifu na mwenye uzoefu. Aliyekuwa mbunge wa Geita Constatine Kanyasu ambaye  pia amewahi kufanya kazi kwa ukaribu na Lukuvi ameiambia DW.

Lukuvi ambaye amefariki leo asubuhi katika Hospitali ya Benjamin Mkapa, jijini Dodoma, alikuwa Bungeni kwa kipindi cha Saba ikiwa ni tangu Mwaka 1995 ulipofanyika Uchaguzi wa Mfumo wa Vyama Vingi nchini.

Zaidi ya miongo mitatu ya utumishi bungeni

Lukuvi, amekuwa mbunge miongo mitatu na Waziri kwa miaka 31, na pia ni miongoni mwa mawaziri walioaminika na awamu tatu za tawala tafauti katika kuongoza wizara kadhaa, ikiwemo ile ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, ikielezwa kuwa alikuwa na uzoefu nayo.

Hilo na mengine vilimfanya Lukuvi kuwa miongoni mwa wabunge wakongwe katika bunge la 13, Mbunge wa Kilolo, Rita Kabati, amezungumzia Lukuvi na kusema ni miongoni mwa viongozi waliofia nchi.

Lukuvi anatajwa kama mwanasiasa aliyelelewa na kukulia ndani ya CCM, akianzia  Umoja wa Vijana (UVCCM) na kuingia bungeni mwaka 1995. Ameshika nafasi mbalimbali za uwaziri ikiwamo Waziri wa Sera, Uratibu,Bunge mpaka mauti yanamfika.

DW Dar es Salaam

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW