1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

WFP yasema bado msaada kwa Gaza ni mdogo

17 Oktoba 2025

Shirika la Mpango wa Chakula la Umoja wa Mataifa, WFP limesema limeweza kusambaza kwa wastani wa takriban tani 560 za chakula kwa siku Gaza tangu usitishaji mapigano kati ya Israel na Hamas ulipoanza kutekelezwa.

Gaza Khan Yunis 2025 | Msaada wa Shirika la Mpango wa Chakula Duniani
Raia wa Palestina abeba msaada wa WFP katika ukanda wa GazaPicha: Hani Alshaer/Anadolu/picture alliance

Msemaji wa shirika hilo la WFP Abeer Etefa, amewaambia waandishi wa habari mjini Geneva kwamba bado kiwango cha msaada kiko chini ya kile kinachohitajika lakini wanaendelea kupiga hatua.

Etefa amesema usitishwaji wa mapigano umefungua fursa ndogo ya kuingiza msaada na WFP inasonga mbele kwa haraka kuongeza msaada wa chakula na kufikia familia ambazo zimevumilia miezi ya kufungwa kwa vivukio, kupoteza makazi na baa la njaa.

Hata hivyo WFP imesema bado haijaanza usambazaji katika mji wa Gaza City, na kusema hilo limesababishwa na kuendelea kufungwa kwa vivuko viwili vya mpaka, Zikim na Erez, huku Israel ikidhibiti kaskazini mwa eneo hilo ambako mzozo wa kibinadamu ni mkubwa zaidi.

Misafara ya misaada bado inashindwa kusambaza msaada Gaza

Ingawa kiwango kidogo cha bidhaa za lishe bora kimefika kaskazini, misafara ya misaada bado haiwezi kupeleka kiwango kikubwa cha chakula katika eneo hilo, pamoja na maeneo mengine.

Wapalestina wakirejea katika ukanda wa GazaPicha: Bashar Taleb/AFP

Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kuratibu Misaada ya Kiutu, OCHA, imesema malori 950 yaliingia Gaza jana Alhamisi ikijumuisha kutoka sekta ya biashara, michango ya nchi na mfumo unaoratibiwa na Umoja wa Mataifa, kupitia vivuko vya Kerem Shalom na Kissufim, ikinukuu takwimu za mamlaka ya Israel inayosimamia masuala ya kiraia katika maeneo ya Palestina COGAT, zilizowasilishwa kwa wapatanishi.

Hamas yataka hatua zaidi ya makubaliano kutekelezwa

Huku hayo yaijiri, Kundi la Hamas, leo limetoa wito kwa wapatanishi katika mzozo wake na Israel, kushinikiza kuchukuliwa kwa hatua zinazofuata chini ya makubaliano ya kusitisha mapigano ikiwa ni pamoja na kufungua mipaka, kuingizwa kwa misaada, kuanza ujenzi mpya, kuanzisha utawala na kukamilisha kuondoka kwa vikosi vya Israel Gaza.

Wataalamu wa Uturuki wasubiri idhini ya Israel kuingia Gaza

Makumi ya wataalamu wa Uturuki waliotumwa na nchi yao kusaidia kutafuta miili katika ukanda wa Gaza kwa sasa wako kwenye mpaka wa Misri, wakisubiri idhini kutoka kwa serikali ya Israeli. Haya ni kwa mujibu wa afisa mmoja wa  Uturuki aliyeliarifu shirika la habari la AFP.

Afisa huyo amesema timu ya maafisa 81 wa taasisi ya shughuli za utafutaji na uokoaji wanasubiri mpakani katika upande wa Misri lakini haijabainika wazi ikiwa Israel itairuhusu timu hiyo kuingia Gaza.

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW