1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroIsrael

WHO yalaani shambulio la Israel dhidi ya hospitali Gaza

3 Januari 2024

Shirika la Afya Duniani WHO limeikosoa Israel kufuatia mashambulizi iliyoyataja kuwa "yasiyokubalika" kwenye hospitali moja katika mji unaokabiliwa na mashambulizi wa Khan Younis kusini mwa Ukanda wa Gaza.

Mzozo wa Ukanda wa Gaza
Mzozo wa Ukanda wa Gaza Picha: Mohammed Dahman/AP Photo/picture alliance

Kulingana na Shirika la Hilali Nyekundu la Palestina, angalau raia watano wameuawa katika shambulio hilo la hapo jana. 

"Niko hapa katika Hospitali ya Al Amal. Ni kituo kinachomilikiwa na Shirika la Hilali Nyekundu ya Palestina na nembo yake imechorwa kwenye paa. Lakini masaa wawili tu yaliyopita, eneo hili limeshambuliwa na watu watano wameuawa akiwemo mtoto mchanga. Hakuna mtoto yeyote duniani anayepaswa kuuawa, hasa akiwa kwenye hifadhi ya shirika la kibinadamu. Vita hivi lazima visitishwe. Nyuma yangu unaweza tu kuona nepi. Hii ilikuwa nafasi wanakoishi watoto, na unaweza kuona damu kwenye sakafu. Dunia inapaswa kughadhabishwa. Leo hii mtoto na watu wengine wanne wameuawa katika eneo ambalo linapaswa kuwa salama. Hakika, hakuna eneo salama Gaza na ulimwengu unapaswa kuwa na aibu, " amesema Gemma Connell, msemaji wa Shirika la Umoja wa Mataifa la misaada ya kiutu, OCHA.

Jumla ya watu 14,000 walikuwa wamelazwa katika hospitali hiyo ya al-Amal lakini kwa sasa wengi wao wameondoka. Kulingana na Wizara ya Afya inayodhibitiwa na Hamas, vita vya huko Gaza tayari vimesababisha vifo vya jumla ya watu 22,313.

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW