1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

WHO yaonya kuhusu "kingamwili" ya virusi vya corona

Sekione Kitojo
26 Aprili 2020

Idadi ya waliofariki duniani  kutokana na janga la  virusi  vya corona imepanda na  kupindukia watu 200,000 leo Jumapili,(26.04.2020)

BdTD Gazastreifen Coronavirus Kostüm
Picha: AFP/M. Abed

Wakati  huo huo shirika la  afya ulimwenguni WHO likionya dhidi ya "kuwapo kwa hati za uimara ya mwili" kwa wagonjwa wanaopona, kunakoonekana  kuwa ni chombo cha mataifa  kujitayarisha  kufungua uchumi wao.

Wagonjwa wanapona , lakini WHO inaonya kuhusu kufikiria kuwa walioambukizwa hawatapata maambukizi mapyaPicha: picture-alliance/AA/C. Bressan

WHO inapinga, "hati"  hizo kwasababu  kupona  kutokana  na maambukizi  ya  virusi vya corona  huenda  kusimlinde mtu  kutokana na  maambukizi tena.

"Kwa sasa  hakuna  ushahidi  kwamba  watu  ambao  wamepona kutokana  na  maambukizi  ya  COVID-19 na  wana chembe cha kingamwili  wana uwezo  wa  kulinda  dhidi  ya  kupata  maambukizi mengine," shirika  hilo  la afya la  umoja wa  Mataifa limesema  katika taarifa.

Wakati  huo  huo  mamia ya  mamilioni  ya  Waislamu  duniani  kote hawakuingia  katika misikiti  katika  siku  ya  pili  ya  mwezi mtukufu wa  Ramadhani na  kuepuka  kula  pamoja  kwa  makundi  katika familia  wakati  wa iftar kwasababu  ya  sera za kutokaa pamoja  na kuweka  umbali kati  ya  mtu  na  mtu.

Na Waaustralia  na  New Zeland wameadhimisha  siku  ya  Anzac bila  ya  magwaride  ya  kawaida  pamoja  na  sherehe  za umma kuadhimisha  wanajeshi waliofariki  katika  vita. Badala  yake, chini ya  utaratibu wa  watu kukaa  mbali  mbali, watu  walikaa nje ya nyumba  zao  usiku.

Mwezi wa ramadhan umeanza Waislamu wamejitenga na kula wengi pamojaPicha: picture-alliance/AP Photo/A. Naveed

Hata wakati  serikali  kutoka   Sri Lanka  hadi  Ubelgiji  mpaka Marekani  zikianza  kuelekea  katika  kufungua  nchi  zao kwa  kiasi fulani, janga  la  virusi  vya  COVID-19 bado  limesababisha  karibu nusu ya  binadamu  kuwa  katika  aina  fulani ya  kuzuiwa  kutembea bila  vizuwizi au kutakiwa  kuwa  katika  majumba yao.

Maambukizi yamepanda

Jumla  ya  maambukizi  duniani  kote  imepanda  na  kufikia  watu milioni 2.86 na  vifo vimefikia  watu 200,000, ikiwa  ni  mara  mbili tangu  tarehe  10 mwezi  Aprili, kwa  mujibu wa idadi  iliyokusanywa na  shirika  la  habari  la  AFP.

Ulaya, eneo  ambalo  limeathirika  mno , limerekodi  vifo 122,171 vinavyotokana  na  virusi  vya  corona.

Idadi  nchini  Marekani  imepanda  kwa  watu 2,494  katika  kipindi cha  masaa 24 na  kufikia  vifo 53,511. Idadi ya  maambukizi  ya virusi  vya  corona  nchini  Marekani  imepanda  kwa  karibu  watu 46,000  hadi  936,293  tangu  Ijumaa.

Nchini  Italia , idadi ya  vifo  vinavyotokana  na  ugonjwa  wa COVID-19 imepanda  hadi  26,384; Uhispania  22,902 , Ufaransa 22,614 na  Uingereza 20,319.

Katika baadhi ya nchi watu wameanza kurejea katika maisha ya kawaidaPicha: AFP/C. Khanna

Dunia  inabaki ikisubiri  wakati makampuni  na  serikali  zinapiga mbio kutengeneza  dawa  na, hatimaye , kupata  chanjo  dhidi  ya virusi  hivyo, ambavyo  vilizuka  kwanza  nchini  China  mwishoni mwa  mwaka  2019.

WHO imeonya  jana  Jumamosi kuwa  watu  ambao  wamethihirika kuwa  wameambukizwa  na  wakapona  kutokana  na  maambukizi hayo  hawawezi  kuwa  na  uhakika  kwamba  hawataambukizwa tena  na  virusi  vya  corona.

Onyo  hilo limetolewa  wakati  baadhi  ya  nchi  zikijitayarisha kufungua  uchumi  wake kwa matumaini  kuwa  wale  waliambukizwa miili  yao itakuwa  na  uwezo wa  kujihami  dhidi  ya  maambukizi mapya. Waziri  mkuu  wa  Ufaransa  Edouard Philippe  kwa  mfano siku  ya  Jumanne atawasilisha  mkakati  wa  taifa  wa  kujitoa kutoka katika  kufungwa  nchi  hiyo  kutokana  na  virusi  vya corona, ofisi  yake  imeliambia  shirika  la  habari  la  nchi  hiyo AFP.

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW