Ruto na Samia kujadili kuhusu biashara na uwekezaji
4 Mei 2026
Viongozi hao wamekuwa na mazungumzo ya ana kwa ana ikulu jijini Dar es salaam kabla ya kujumuika na hadhira inayojumuisha viongozi wa kada mbalimbali kujadiliana masuala ya biashara na uwekezaji.
Jukwaa hilo ni uwanja unazingatiwa na pande zote mbili kwa ajili ya kusaka majawabu ya pamoja ya namna bora ya kuvutia uwekezaji na kupunguza kile kinachotajwa kama vikwazo vya kikodi vinavyorudisha nyuma shughuli za kibiashara miongoni mwao.
Katika kipindi cha mwaka 2022 mawaziri wa uwekezaji wa pande zote mbili walitambua vikwazo 68 na kati yake 54 vilitafutiwa majawabu kabla vingine vinne kuondolewa Oktoba mwaka jana.
Hadi wakati huu pande hizo mbili zinakabiliwa na vikwazo vipatavyo 10, na wataalamu wa mambo wanaamini kuwa kupitia kongamano hilo ambalo pia limewajumuisha wawekezaji wa sekta binafsi vinaweza kupatiwa majawabu.
Paternus Niyegire ambaye ni mchambuzi wa siasa, uongozi na diplomasia anasema pande hizo zina nafasi kubwa ya kuendelea kufungua wigo wa kibiashara iwapo zitazidi kuonyesha nia ya kuondoa vikwazo vilivyosalia.
Anaamini kuwa, kuendelea kupunguzwa vikwazo hivyo kutoka 58 vilivyokuwa awali hadi kufikia 10, kunatoa matumaini juu ya uwezekano wa kumalizika mivutano ya kibiashara iliyoko.
Mazungumzo yananuiwa kutuliza mivutano ya kibiashara
Licha ya maingiliano ya karibu yaliyopo kati ya Kenya na Tanzania, mara kadhaa nchi hizo zimekuwa zikijikuta zikitumbukia katika mivutano ya kibiashara hali ambayo wengi wanaitazama imesababisha pia kuzorotesha ustawi wa kibiashara miongoni mwa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki yenye nchi wanachama nane.
Mapema akizungumza katika ufunguzi wa kongamano hilo kabla ya kuwasili marais hao, Waziri wa nchi ofisi ya rais anayehusika na masuala ya mipango na uwekezaji Kitila Mkumbo alisema kwa namna yoyote ile mataifa hayo hayawezi kukwepana katika maingiliano yao.
Hivyo alisisitiza njia bora ya kuungana na kushirikiana katika kuziendeleza fursa zinazopatikana katika maeneo husika ili kuharakisha shabaha ya kukuza maendeleo. Aliitaja sekta binafsi kama uti wa mgongo wa pande hizo mbili kukimbia katika biashara.
"Kwa hiyo jukwaa hili ni muhimu kwa sababu linawaleta katika chumba kimoja watunga sera na sekta binafsi, hivyo ningependa kuwatia moyo kuzingatia mambo yanayotoa matokeo yenye uhaliisi”
Ndani yaJumuiya ya Afrika Masharikimataifa hayo mawili yanatazamwa kama mhimili wa kibiashara na kwamba tangu mwaka 2020 hadi 2024, nchi hizo zilichangia asilimia 40 ya biashara yote katika jumuiya hiyo.