1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

William Ruto aapishwa kuwa Rais wa Kenya

13 Septemba 2022

William Samoei Ruto ameapishwa kuwa rais wa tano wa Jamhuri ya Kenya. Dkt Ruto amekula kiapo katika uwanja wa Kasarani mjini Nairobi.

Präsidentschaftswahl in Kenia
Picha: Billy Mutai/AA/picture alliance

Hafla ya kuapishwa kwa Ruto imesimamiwa na msajili wa idara ya mahakama Anne Amadi na kushuhudiwa na jaji mkuu Martha Koome.

Hafla ya kuapishwa kwa Ruto imehudhuriwa na viongozi mbalimbali duniani akiwemo Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan, Yoweri Museveni wa Uganda, Paul Kagame wa Rwanda, Evariste Ndayishimiye wa Burundi, Felix Tshisekedi wa Jamhuri ya Demokrasia ya Congo, Salva Kiir wa Sudan Kusini, Emmerson Mnangagwa wa Zimbabwe, Nana Akufo-Addo wa Ghana, Lazarus Chikwera wa Malawi na Waziri Mkuu Ethiopia Abiy Ahmed.

Maelfu ya watazamaji wamefurika katika uwanja wa michezo wa Kasarani mjini Nairobi kushuhudia William Ruto akiapishwa kuwa rais wa Kenya baada ya ushindi wake mwembamba katika mchuano mkali wa uchaguzi wa rais ambao kwa sehemu kubwa ulifanyika kwa amani. 

Ruto amekula kiapo cha kuwa rais wa tano wa Kenya na kumrithi Rais Uhuru Kenyatta aliyemaliza mihula miwili ya miaka mitano kila mmoja.

Mapema leo, watu kadhaa walijeruhiwa wakati umati wa watu ulijaribu kuingia kwa nguvu uwanjani hapo huku picha za televisheni zikionyesha watu kadhaa wakiangukiana na kukanyagana katika mojawapo ya malango.

Polisi iliwaambia Wakenya kufuatilia hafla hiyo majumbani mwao baada ya uwanja huo wenye uwezo wa kuwa na watu 60,000 kujaa kabla ya alfajiri leo.